Serikali imesema Kongani ya Buzwagi itachochea ukuaji uchumi wa nchi

Yaipongeza Barrick kwa kufunga mgodi kwa viwango bora

 

Na MWANDISHI WETU

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais  Mipango na Uwekezaji, Dkt. Pius Stephen Chaya, amesema kuwa Kongani ya Viwanda ya Buzwagi Special Economic Zone inatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha uchumi wa Mkoa wa Shinyanga na Taifa kwa ujumla, kutokana na mpango wake unaotoa fursa mbalimbali za uwekezaji.

Dkt. Chaya ameyasema hayo baada ya kufanya  ziara ya kikazi  ya kutembelea kongani hiyo iliyopo katika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga ambapo pia aliipongeza kampuni ya Barrick kwa ufungaji wa mgodi wa Buzwagi kitaalamu na kufanya eneo hilo kuwa la kuvutia kwa wawekezaji.

“Nimefurahi kusikia kuwa eneo hili limetengwa miongoni mwa maeneo sita ya uwekezaji, ambapo mnapanga kujenga vyuo vya ufundi, makazi, viwanda na miundombinu mingine muhimu. Hivyo basi, Buzwagi ni eneo sahihi kabisa kwa uwekezaji na limepangiliwa vizuri na wadau wote wanaosimamia eneo hili ikiwemo Kampuni ya Barrick,” alisema Dkt. Chaya.

Ameongeza kuwa azma ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha Watanzania wanakuwa  na maisha bora na aliwataka wananchi kuchangamkia fursa hii ya kongani kubadilisha maisha yao.

“Serikali inapenda kuona Wananchi wa Kahama na Tanzania katika sekta zote ikiwemo , akina mama lishe, wasomi na hata wasiokuwa wasomi wanapata ajira na fursa za kipato kupitia uwekezaji huu mkubwa  katika kanda hii ya ziwa”, amesisitiza.

Dkt. Chaya aliwataka viongozi pamoja na wadau wote wa maendeleo kuhakikisha wanashirikiana kwa pamoja ili kutimiza dhamira na maono ya Mheshimiwa Rais.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Frank Nkinda aliyekuwa katika ziara hiyo alieleza kuwa Kongani ya Viwanda ya Buzwagi ina vigezo vyote vinavyohitajika kuwavutia wawekezaji, ikiwemo mazingira rafiki ya uwekezaji, eneo kubwa pamoja na uwepo wa uwanja wa ndege unaorahisisha  usafiri.

“Serikali inaendelea kufungua wigo kwa ushiriki wa watanzania katika sekta ya madini na kuongeza manufaa ya rasilimali madini kwa kutenga eneo hili maalumu la uwekezaji la ulipokuwa Mgodi wa uchimbaji mkubwa wa madini ya dhahabu la Barrick Buzwagi lenye ukubwa wa ekari 1331,  ni kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya kuzalisha bidhaa za migodini na kusema tayari viwanda sita vimekwisha jengwa huku wamiliki wa viwanda 15 wakionesha nia ya kujenga viwanda katika eneo hilo.

Ametoa wito kwa watanzania kuchangamkia fursa zilizopo katika kongani hiyo  ili kukabiliana na changamoto za ajira kwa manufaa ya mtu mmoja mmoja na manufaa ya taifa.

Naye Meneja Ufungaji wa Mgodi wa Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi, alisema kwa sasa kuna mwitikio  mkubwa kwa wawekezaji Kuhitaji kuwekeza Katika Kongani hiyo kutokana na  kukidhi vigezo vyote vinavyovutia wawekezaji. 






Serikali imesema Kongani ya Buzwagi itachochea ukuaji uchumi wa nchi Serikali imesema Kongani ya Buzwagi itachochea ukuaji uchumi wa nchi Reviewed by Gude Media on January 12, 2026 Rating: 5

Boxed Width - True/False

True