Rais Dk. Samia Awasili nchini Urusi kwa ziara ya Kuimarisha Ushirikiano na fursa za Uwekezaji

 


Na Beda Msimbe, TBN, Moscow

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ziara ya Kitaifa, nchini Urusi

Katika ziara hiyo ya kihistoria ikifanywa kwa mara ya pili katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Urusi, ya kwanza ilikuwa ni miaka ya 1960 iliyofanywa na baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Rais Samia anaendeleza kampeni kubwa ya kuhakikisha Tanzania inanufaika pia kiuchumi na uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali

Kwa mujibu wa shughuli atakazofanya Rais Samia akiwa nchini humo kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi.

Rais amekuja kuiweka Tanzania katika ramani ya uwekezaji kwa ushiriki wake katika mkutano mkubwa wa uwekezaji jijini St Petersburg pia kuona namna ya kutengeneza rasilimali watu ambayo taifa inahitaji sana katika kufanikisha utekelezaji wa dira ya maendeleo ya 2050. 

Alipowasili nchini humo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, Jijini Moscow saa mbili na dakika 25 usiku , japo jua bado lilikuwa linawaka, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokea heshima ya wimbo wa Taifa pamoja na gwaride.

Rais Samia alipokewa uwanjani na Waziri wa Maendeleo ya Uchumi wa Shirikisho la Urusi Mhe. Maxim Reshetnikov. 

Kwa mujibu wa ratiba leo asubuhi ataanza na kuweka shada ka maua kwa kaburi la askari asiyejulikana kabla ya kwenda Ikulu ya Kremlin kwa mazungumzo na Rais Vladmir Putin.