Kampuni ya Barrick nchini, imeendeleza dhamira yake ya kuibua na kukuza vipaji vya vijana wasomi wa vyuo vya elimu ya juu na kati nchini ili waweze kukabiliana na mabadiliko yanayoendelea kutokea duniani na kuhimili ushindani katika soko la ajira sambamba na kuweza kujiamini kutumia ujuzi na taaluma zao kujiajiri kwa ajili ya kujenga mustakabali endelevu.
Hayo yameeleza na Afisa Raslimali Mwandamizi wa Barrick Tanzania, Elibramack Joel akiongea na Wanafunzi wa Vyuo vikuu vilivyopo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa kongamano la kuwajengea uwezo wa kuhimili ushindani wa ajira na kujiajiri lililoandaliwa na taasisi ya kuchipua na kuendeleza vipaji vya uongozi kwa vijana (AIESEC) lililofanyika katika Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) kampasi ya Mlimani kwa udhamini wa Barrick ambayo inaendesha shughuli zake nchini kwa ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga Minerals.
Joel, pia aliwaeleza wasomi hao shughuli za kampuni ya Barrick nchini na mkakati wake wa kuinua vipaji vya vijana sambamba na kuwezesha wanafunzi wa kike kusoma masomo ya sayansi ili wapate fursa ya kupata ajira katika sekta ya madini ambayo kwa sasa asilimia kubwa inatawaliwa na wanaume.
Kongamano hilo kubwa limehusisha makampuni mengine makubwa ya ndani na nje kwa ajili ya kuwanoa wanafunzi kuhusiana na mabadiliko ya teknolojia,ajira na kujiajiri wenyewe pindi wamalizapo masomo yao.
Wanafunzi wengi walioshiriki kongamano hilo walipata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusina na jinsi ya kupata fursa ya ajira katika makampuni yaliyodhamini kongamano hilo.
Mbali na kudhamini kongamano hilo Barrick pia mwaka jana imetoa udhamini kwa wanafunzi 5 kutoka Chuo Kikuu cha Dares Salaam kwenda kusoma shahada ya kwanza ya elimu ya Madini na Jiolojiakatika Chuo Kikuu cha Jahannesburg nchini Afrika ya kusini kupitia program yake ya kuwezesha wasomi vijana inayotekelezwa kanda ya Afrika Mashariki na kati.





