Sidde Apiga Marufuku Wanachama CCM Ilala Kuanza Kampeni Mapema


Na MWANDISHI WETU

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ilala, Saidi Sidde, amepiga marufuku wanachama wa chama hicho walioanza kufanya kampeni za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Chama kabla ya wakati na kuwataka kusitisha haraka.

Sidde ametoa kauli hiyo katika Kata ya Msongola, Wilaya ya Ilala, wakati wa kupokea taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya Chma kwa kipindi cha kuanzia Januari hadi Juni 2026. 

"CCM Wilaya ya Ilala inatoa onyo kwa wanachama wote walioanza kufanya kampeni za kugombea uongozi ndani ya chama waache mara moja. Hakuna anayejua kesho; hivyo wasubiri muda rasmi utakapofika na filimbi itakapolia," amesema.

 Pia amewataka wanachama kuepuka kujenga uadui kutokana na siasa au kujiona kuwa wao ni muhimu kuliko wengine na kusisitiza kuwa siasa zinahitaji mshikamano na ushirikiano.

Sidde amewataka viongozi kusimamia maeneo yao kwa weledi na kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

 Akizungumzia kuhusu uhai wa CCM, Sidde amewataka viongozi kuendelea kuimarisha vikao vya matawi na mashina pamoja na kuijenga Chama na jumuiya zake, zikiwemo Wazazi, Umoja wa Vijana wa CCM, Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT).

Amesema  juhudi hizo zitasaidia kuongeza wanachama wapya, kuwasajili katika mfumo wa kielektroniki na kuhakikisha wanalipa ada zao kwa wakati.

 "Naagiza kila jumuiya isimamie kikamilifu majukumu yake sambamba na kushughulikia kero za wananchi. UWT ifuatilie wanawake waliopata mikopo ya Serikali, Jumuiya ya Wazazi ifuatilie maendeleo ya sekta ya elimu shuleni, ikiwemo hali ya masomo kwa wanafunzi na kudhibiti michango holela mashuleni," alisema.

 Akizungumzia Kata ya Msongola, Sidde amewapongeza wanachama wa CCM kwa kukipatia Chama ushindi mkubwa katika uchaguzi, ambapo walimchagua Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mbunge wa Jimbo la Kivule, Ojambi Didas Masaburi na Diwani wa Kata ya Msongola, Magdalena Thomas.

Aidha Sidde amewataka wanachama wa CCM kuendelea kudumisha umoja na mshikamano na kushirikiana kwa karibu katika kuimarisha chama na Serikali.