Mabinti kuchukua fomu za kuomba wachumba zao kuwalipia mahari
Na MWANDISHI WETU
Al-Hikma Foundation waandaaji wa Mashindano Makubwa ya Kuhifadhi Quraan ya Mabara yote, imetangaza neema ya kugharamia ndoa 130 kwa vijana wasiyo kuwa na uwezo wa kulipa mahari.
Akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam, Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Shekh Nurdeen Kishk, amesema awamu hii mwanamke anaye taka kuolewa ndiye atakaye chukua fomu ya kuomba mwenza alipiwe mahari na kuozeshwa.
Kishk amesema fomu za kuomba kulipiwa mahari na kuozeshwa kwa mabinti hao zitaanza kutolewa machi 9 hadi Aprili 10 mwaka huu katika ofisi za Al-Hikma, Temeke, Dar es Salaam.
“Wanawake wanaotaka kuolewa awamu hii watakuja Al-Hikma kuwachukulia fomu wachumba zao, zijazwe na zirudishwe kusubili hatua nyingine ikiwemo kifanyiwa usahili", amesema.
Kishk amesema awali wanaume ndiyo walikuwa wakichukua fomu hizo ambazo zina masharti yanayo mfanya mtu kukidhi vigezo vya kusaidiwa kufunga ndoa, kikiwemo kigezo cha kuwa raia wa Tanzania.
“Huu ni mwaka wanne Al-Hikma Foundation tumekuwa tukisaidia jamii kuozesha vijana wa kike na wakiume, mpaka sasa tumeozesha ndoa 370,” amesema Kishk.
Amesema awamu hii Al-Hikma Foundatio imejipanga kuozesha ndoa 130 lakini Rais wa Taasisi hiyo Sheikh Sharif Al Ahadal ataongeza ndoa 30.
Pia Kishk amesema miongoni mwa vigezo hivyo ni lazima mwanaume awe na njia za kupata kipato, Kitambilisho cha Taifa (NIDA), barua kutoka kwa Imamu wa msikiti anapoishi.
“Pia mwombaji awe ameposwa na mwanaume awe ameposa, awe mke wa kwanza, mwanaume asiwe unaongeza mke wa pili Kama una mke unataka kuongeza basi mahari utalipa mwenyewe,” amesema.
Vigezo vingine ni kukubali ndoa kufungwa jijini Dar es Salaam, wazazi wa mwanamke waridhie ndoa hiyo.

