HALMASHAURI KUU YA CCM YAMPITISHA MASABURI KUGOMBEA UBUNGE JIMBO LA KIVULE


Na MWANDISHI WETU

CHAMA  Cha Mapinduzi (CCM) kimemteua aliyewahi kuwa Naibu Meya wa  Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Ojambi Masaburi kuwa  mgombea ubunge wa Jimbo la Kivule,  jijini Dar es Salaam katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu.


Masaburi aliongoza katika mchakato wa kura za maoni ndani ya Chama,  ametangazwa kuwa mgombea ubunge katika jimbo hilo  baada ya Kamati ya Halmashauri Kuu ya CCM, kuchuja majina ya wagombea ubunge wake ambao watapeperusha bendera katika uchaguzi huo.


Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, CPA Amoss Makalla ametangaza majina ya wagombea ubunge kwa majimbo yote kupitia CCM, ambapi Jimbo la Kivule mgombea ubunge aliyepitishwa na Chama  ni Ojambi Masaburi .


Masaburi atachukua fomu ya uteuzi  kugombea ubunge na kisha kuirejesha katika Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) na kusubiri kuanza kampeni ya kuomba kura kwa wananchi katika jmbo la hilo.


Kivule ni jimbo jipya ambalo limepatikana baada ya Tume Huru ya Uchaguzi (INEC),  kuligawa Jimbo la Ukonga na kupatikana majimbo mawili ya uchaguzi  ambayo ni  Ukonga na Kivule.