Uongozi mpya UKUTA Wakabidhiwa Rasmi Ofisi


Na MWANDISHI WETU

UONGOZI mpya wa  Taasisi ya  Usanifu wa Kiswahili na Ushairi Tanzania (UKUTA) , umekabidhiwa rasmi ofisi  kutoka kwa uongozi uliopita  baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika  Julai 11 mwaka huu. 

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Anatouglou, jijini Dar es Salaam, Makao Makuu ya UKUTA,  Mwenyekiti wa  taasisi hiyo  taifa,   Hussein  Jimbika, amesema wamejipanga kusimamia kikamilifu  usanifu wa lugha ya Kiswahili na ushairi nchini.

Amesema UKUTA itaendelea kuenzi jitihada  kubwa za viongozi na waasisi  wa taasisi hiyo, hususan Baba wa Taifa  hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambaye ndiyo mtu wa kwanza kuunda chombo hicho, kabla ya uhuru kwa kushirikiana na  hayati Abeid Aman Karume na  Sheikh Amri Abeid Karuta.

Ameeleza UKUTA  ilitoa mchango mkubwa katika kufanikisha  taifa kupata  uhuru na kwamba  uongozi  wa taasisi hiyo  utaendelea kufuata nyendo zao kuhakikisha  safari  ya kuenzi Kiswahili inafanikiwa.

“Wazee hawa walikuwa na makusudio makubwa ya Kiswahili  kuwa ni nyenzo muhimu ya kupata uhuru na ustawi wa taifa", amesema. 

Hivyo Uongozi mpya tutashirikiana na wenzetu kuhakikisha lengo la waasisi hawa linaendelewa na kufikiwa katika kukuza Kiswahili,”amesema Jimbika.

Jimbika amesema  lengo lingine ni kuongeza usajili wa wanachama kwani mpaka sasa UKUTA inawachama 2050 tu.

Katibu Mkuu wa UKUTA, Abubakary Kiaibamba, amewarika wanachama katika ofisi za makao makuu ya taasisi  hiyo zilizopo katika jengo la  Anatouglou kwa  uratibu wa shughuli zote  za taasisi na kujisajili .

“Malengo yangu ni kuhakikisha tunakifanya Kiswahili kuwa bidhaa. Hii ndiyo kazi anayoifanya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Tutahakikisha  vitabu vinaandikwa, mashairi yanatungwa na  tunawakomboa  washairi kiuchumi kupitia  kazi zao,” amesema Kiaibamba.

Akikabidhi nyaraka za ofisi, Katibu Mkuu mstaafu Hassan Ligile, ameupongeza uongozi mpya kushinda katika uchaguzi wa kidemokrasia uliofanyika na kwamba wataendelea kutoa ushirikiano  kuhakikisha UKUTA inasonga mbele huku akijivunia mafanikio yaliyopatikana  chini ya uongozi wake.