Meya Temeke: Uvumilivu wangu utakuwa sifuri kwa mtu atakayechelewesha ukamilifu wa miradi



Na Mwandishi wetu

MEYA wa Manispaa ya Temeke, jijini Dar es Salaam,  Uzairu Athumani, amesema atakuwa na uvumilivu sifuri kwa mkandarasi  atakayechelewesha ukamilishaji wa miradi ya maendeleo.                

Akizungumza ofisini kwake, Meya Uzairu amesema atakayeshindwa kutekeleza mradi kwa wakati uliopangwa atachukuliwa hatua kwa haraka.      

Amesema atakuwa na uvumilivu sifuri kwa mkandarasi atakayepewa mradi wa kujenga miundombinu akiwemo barabara.

"Kwa mkandarasi yeyote atakayeshindwa kukamilisha mradi kwa wakati atachukuliwa hatua haraka sana," amesema Meya Uzairu.  

Uzairu amesema hatakuwa na uvumilivu hata kidogo kwa mkandarasi atakayejenga barabara chini ya kiwango na miradi mingine na kuahidi kufuatilia  kwa  ukaribu  kuhakikisha miradi ya maendeleo inakamilika kwa wakati.  

Amesema  atakuwa makini katika suala la ukusanyaji wa mapato ili kuhakikisha Manispaa inaendelea kuwa kinara katika ukusanyaji wa mapato.  

Amefafanua kuwa matarajio yake nikuona Temeke inakusanya mapato mengi, na elimu ya ulipaji kodi inatolewa na  iwe rafiki kwa kila mmoja kwa maana mfanyabiashara 

Amesema elimu ikitolewa kwa  kila mlipa kodi itaweze kuelewa umuhimu wa kulipa kodi kwani hali ya uchumi wa wananchi wetu unafahamika.   

Amesema kwa mwaka wa fedha 2026, Manispaa ya Temeke inatarajia kukusanya Sh Bilioni 70, ambapo kati ya hizo asilimia 30 zitatumika katika matumizi ya kawaida na asimilia 70 zitatumika kwa shughuli za maendeleo, ikiwemo elimu na miundo mbinu.   

"Mimi na madiwani tumejipanga vizuri, kutunga sheria ndogo kwa ajili ya kuongeza kukusanya mapato,' amesema Meya Uzairu.     

Wakati huo huo, Meya Uzairu amesema atahakikisha ahadi za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, zilizozitoa wakati wa kampeni, Temeke inakuwa ya kwanza kuzitekeza.   

Rais Dkt. Samia alitoa ahadi ambazo zitatekelezwa ndani ya siku 100 tangu kuchaguliwa kwake, Oktoba   29, mwaka huu.      

Meya Uzairu amesema tayari Temeke imeanza kutekeleza kwa asilimia 100 maelekezo ya Serikali kuhusu  kuruhusu maiti kutolewa hospitalini bila kutozwa fedha.     

Amesema pamoja na ahadi nyingine alizotoa Dkt.Samia wakati wa kampeni zake,kwa kushirikiana na mkurugenzi na watendaji wake atahakikisha anasimamia vema  utekelezaji wa ahadi hizo kabla ya kumalizika kwa  siku 100.