Barrick Bulyanhulu Yabadilisha Maisha ya Wananchi Bugarama Kupitia Miradi ya Ufugaji Nyuki na Mazingira


Msalala: Mgodi wa Barrick Bulyanhulu uliopo Halmashauri ya wilaya Msalala mkoani Shinyanga umekuwa ukiwezesha wananchi wanaoishi maeneo yanayouzunguka kuendesha miradi mbalimbali ya kujikimu kimaisha na upandaji miti ya matunda na mbao ,hali ambayo imefanikiwa kujenga uhusiano mzuri na jamii sambamba na uwepo mwamko wa utunzaji wa mazingira na vyanzo vya maji.

Kikundi cha Ufugaji nyuki na utunzaji wa Mazingira cha Twikondele, kilichopo katika Kijiji cha Buyange Kata ya Bugarama ni moja ya wanufaika wa uwezeshaji kutoka mgodi wa Bulyanhulu hatua iliyokisaidia kukuza shughuli za kiuchumi na kuweza kujitegemea na kuishi maisha bora.

Katibu wa kikundi hicho, Daniel Samson akitoa taarifa kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Mwang'onda wakati mwenge ulipotembelea kikundi hicho kukagua shughuli za ufugaji nyuki pamoja na vitalu vya miche ya miti mbalimbali ikiwamo ya matunda,alisema kupitia ufadhili wa mgodi wa Barrick Bulyanhulu wamepata mafanikio makubwa na wanakikundi na wananchi wengine katika kata zinazozunguka mgodi wanaendelea kunufaika kupitia uwezekezaji huo wa Kampuni ya Barrick ambayo kwa hapa nchini inaendesha shughuli zake kwa ubia na serikali kupitia kampuni ya Twiga.

Samson amesema kikundi hicho chenye wanachama 10 kilianza shughuli za ufugaji nyuki mwaka 2015 kikiwa na mizinga saba pekee, hali ambayo ilifanya uzalishaji wa asali kuwa mdogo hadi mwaka 2023 walipopata uwezeshaji wa shilingi milioni 25 kutoka mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu fedha ambazo zilitumika kununua mizinga ya kisasa ya kufugia na kuongeza idadi ya mizinga kutoka saba hadi 117.

Amesema kupitia uwekezaji huo uzalishaji wa asali uliongezeka ambapo sasa wanachama wananufaika kwa kupata fedha za kuboresha maisha yao kupitia kuuza asali sambamba na kuzalisha miche ya mazao mbalimbali.

Kwa upande wake Afisa Mwandamizi wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira kutoka mgodi wa Barrick Bulyanhulu,Zuwena Senkondo alisema katika kufanikisha utekelezaji wa mkakati endelevu wa kampuni na kuunga mkono jitihada za serikali za kuwakwamua wananchi kiuchumi,mgodi unafanya kazi na vikundi mbalimbali vya wananchi na kuviwezesha kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ya ufugaji wa nyuki na uoteshaji wa miche miti ya matunda na mbao kwa ajili ya kutunza mazingira na kujiongezea kipato.

Senkondo pia amesema kuwa mgodi umekuwa ukifadhili mafunzo mbalimbali ya wanavikundi kwa ajili ya kuwezesha wanachama wake kujifunza jinsi ya kuendeleza miradi hiyo,mafunzo ambayo yamesaidia wanavikundi kufanya shughuli za ufugaji katika ngazi ya kaya zikiwamo kuku, mbuzi na ng’ombe ili kuongeza vyanzo vya mapato ndani ya familia zao.

Awali, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Mwang'onda, amekipongeza kikundi hicho kwa juhudi zake za kutunza mazingira kupitia uoteshaji wa miche ya miti ikiwamo ya matunda na kuhimiza wananchi kuendelea kupanda na kutunza miti ili kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa nchi yenye mazingira bora na ya kijani.

Mwang'onda pia alitoa pongeza kwa mgodi wa Barrick Bulyanhulu  kwa kuendelea kuwezesha vikundi mbalimbali vya ujasiriamali ambavyo vimekuwa vikisaidia wananchi kuinua hali zao za kiuchumi kupitia shughuli wanazofanya na alitoa ombi kwa mgodi kuendelea kushirikiana na jamii  kupitia kuwezesha miradi ya kuinua maisha ya wananchi na utunzaji wa mazingira.